MBUNGE wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi (CHADEMA), leo anatarajiwa kuanza ziara ya kukijenga chama Kanda ya Nyanda za Juu Kusini.
Akizungumza na Tanzania Daima jana kwa njia ya simu kutoka Mbeya, Sugu
alisema kuwa anaanza ziara ya kichama ya siku tatu mkoani Ruvuma,
ambako atahutubia mikutano ya hadhara.
Mbilinyi maarufu kama ‘Sugu’ alisema kuwa leo atafanya mkutano huko
Madaba na kesho atakuwa mji mdogo wa Mbinga na Jumapili atamalizia mjini
Songea.
"Leo nitaanza ziara ya siku tatu ya kichama mkoani Ruvuma, ambako
nitaungana na viongozi wengine wa Chachema mkoani humo, kuhutubia
mikutano ya hadhara ili kusaka wananchama wapya kutoka Nyanda za Juu
Kusini,” alisema Sugu.
Katika hatua nyingine, Sugu alisema kuwa anashukuru kuona ujenzi wa
barabara kwa kiwango cha lami katikati ya mji wa Mbeya unaendelea
vizuri, jambo linalompa faraja kwamba anatekeleza ahadi zake za
kuwaletea maendeleo wakazi wa Mbeya.
Alisema kuwa anaamini ataweza kuzitimiza ahadi zake zote ndani ya muda
muafaka kutokana na jinsi wananchi na watendaji wa Mbeya wanavyomuunga
mkono.
"Kwa kweli ninafarijika kuona wananchi wa Mbeya pamoja na watendaji wa
serikali wanaweka itikadi pembeni na wanakuwa na lugha moja katika
kutekeleza miradi ya maendeleo,” alisisitiza Sugu.