CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimetishia kuweka
hadharani majina ya mawaziri na wabunge ambao walikuwa tayari kujiunga
na chama hicho.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam,
Mkurugenzi wa Uenezaji wa chama hicho, John Mnyika, alisema Chama cha
Mapinduzi kisitake kuilazimisha CHADEMA iseme ukweli wote juu ya wimbi
kubwa la wana CCM, wakiwemo wabunge na mawaziri ambao wanataka kujiunga
nayo.
Mnyika akijibu taarifa ya CCM iliyotolewa na Katibu wa Uenezi na
Itikadi, Nape Nnauye, alisema kuwa viongozi wengi wa chama hicho tawala
wanajua mchakato mzima uliokuwepo wa wabunge, mawaziri na wana CCM
wengine kutaka kuhamia CHADEMA tangu wakati wa uchaguzi mkuu wa 2010
lakini wakaingiliwa.
Mnyika aliwataka viongozi wa CCM waseme kama wako tayari kupokea
ukweli mchungu wa viongozi wao walio tayari kukihama chama hicho na
kujiunga na upinzani
"Wasitulazimishe kusema. Na kama wanataka waseme kama wako tayari,
tufungue boksi, ikibidi hata nitaje majina ya watu na kwa nini baadaye
walishindwa kujiunga,” alisema Mnyika.
Mnyika alisema imekuwa ni kawaida ya CCM kukanusha kila kitu, na
kumlinganisha Nape na aliyekuwa Waziri wa Habari wa Iraq chini ya
utawala wa Saddam Hussein ambaye alikanusha kila kitu, huku akijua
majeshi ya Marekani yalikuwa yamewazidi nguvu.
"Sisi hatuwashangai wao kukanusha maana hata wakati waliokuwa madiwani
wao wanahama kutoka CCM kuja CHADEMA walikanusha hivihivi, lakini leo
yako wapi, madiwani kuanzia Arusha mpaka Mwanza huko wamehamia CHADEMA,
hivyo hata hili la wabunge na mawaziri atakanusha sana lakini si atulie
asubiri aone,” amesema Mnyika.
Taarifa ya CCM iliyotolewa jana imekanusha madai yaliyotolewa na
Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, Freeman Mbowe, ambaye mwishoni mwa wiki
jana alitangaza katika mkutano mkubwa wa hadhara jijini Arusha kuwa
wabunge 70 na mawaziri kadhaa walikuwa tayari kujiunga na chama hicho
cha upinzani.
Nape alidai kuwa maneno hayo ya Mbowe ni uongo kwa vile hakuna waziri
au mbunge ambaye yuko tayari kuondoka ndani ya CCM na kwamba yametolewa
kwa lengo la kujipatia umaarufu wa bure.
Hoja ya mauaji
Akizungumzia tamko la CCM lililotolewa jana kukanusha tuhuma za
kuhusika na mauaji, Mnyika alikishambulia vikali chama tawala akidai
kimeshindwa, Nape anaficha ukweli juu ya kuhusika kwa baadhi ya viongozi
wake na mauaji hayo.
"Kama angetafakari kabla ya kusema angejua kuwa mpaka sasa viongozi wa
serikali wanaotokana na CCM wako chini ya ulinzi wa polisi kuhusiana na
mauaji ya Mwenyekiti wa CHADEMA Kata ya Usa River. Lakini pia viongozi
na wanachama wa CCM wametajwa kwa majina kuhusika katika tukio la
wabunge wa CHADEMA kukatwa mapanga huko Mwanza. Na mpaka sasa wako chini
ya uchunguzi wa Jeshi la Polisi Mwanza,” alisema Mnyika.
Aliongeza kuwa kuna majina ya viongozi wa CCM waliotajwa kuhusika
katika vitendo vya mauaji na vingine vya utekaji kwa wanachama na makada
wa CHADEMA katika maeneo mbalimbali mathalani wakati wa uchaguzi mdogo
wa Kiteto, Busanda, Biharamulo na kwingine.
Mnyika aliongeza kuwa kama kweli CCM inataka kuonyesha kuwa ina
uchungu na inakerwa na wimbi la mauaji ya kisiasa yanayoendelea nchini,
basi walizungumze suala hilo katika vikao vyao kuielekeza serikali
kutumia sheria ya Inquest Act, sura ya 24 ya sheria za Tanzania ambayo
inaitaka serikali kuchunguza vifo vyenye utata.