MBUNGE wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari (CHADEMA), amesema kuwa
hana nia wala dhamira ya kuchochea na kuhamasisha mgawanyiko katika nchi
kama ambavyo imekuwa ikitafsiriwa na baadhi ya watu.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, juu ya maneno anayodaiwa
kuyatoa Jumamosi kwenye mkutano wa hadhara wa chama chake wakati wa
uzinduzi wa operesheni ‘vua gamba vaa gwanda’ kwenye viwanja vya NMC,
Nassari alidai lengo la hotuba yake lilikuwa kuhimiza serikali na jeshi
la polisi lishughulikie mauaji ya watu na kudai hakulenga kuchochea
vurugu au kumzuia Rais kutekeleza wajibu wake.
"Kumetokea sintofahamu kubwa kuhusu sehemu ya hotuba yangu niliyoitoa;
chama changu siku zote kimekuwa mstari wa mbele kuunganisha umma wa
Watanzania wote kudai haki, umoja, amani na maendeleo ya kweli bila
kujali ukanda, udini wala historia, ningependa ifahamike kuwa sina lengo
wala dhamira ya kuwagawa Watanzania kwa namna yoyote ile kama ambavyo
imekuwa ikitafsiriwa,” alisema Nasari.
Alisema hata kauli ya ufafanuzi iliyotolewa na Mwenyekiti wake wa
Taifa, Freeman Mbowe, kwenye mkutano huo baada ya yeye kuzungumza
iliweka mkazo juu ya msimamo wa CHADEMA wa kuunganisha nguvu ya umma
katika maendeleo ya Watanzania.
"Hata alipohojiwa na vyombo vya usalama kutaka kujua nilimaanisha nini aliwaeleza hivyo,” alisema.
Nassari ametoa kauli hiyo siku moja baada ya jeshi la polisi kudai
linasubiri ridhaa ya Mkurugenzi wa Mashtaka Nchini (DPP) ili waweze
kumfikisha mahakamani pamoja Mwenyekiti wa BAVICHA Taifa, John Heche, na
mwanachama Ally Bananga ambaye alikuwa amehamia CHADEMA siku hiyo ya
mkutano akitokea CCM alikokuwa akishika nyadhifa mbalimbali za uongozi.
Naibu Kamishina wa Polisi, Isaya Mungulu, aliwaeleza waandishi wa
habari juzi kuwa baada ya kuwahoji wamebaini makosa wanayowatuhumu nayo
yanaangukia katika kifungu cha sheria namba 63 b cha kanuni ya adhabu,
sura namba 16 ambapo inahitaji ridhaa ya DPP kabla ya kuyafikisha
mahakamani.
UVCCM wamshukia
UMOJA wa vijana wa Chama cha Mapinduzi (CCM) umemtaka Msajili wa
Vyama vya Siasa nchini, kuviwajibisha baadhi ya vyama ambavyo vinatumia
vibaya uhuru wake.
Katibu mkuu wa umoja huo, Martin Shigela, alisema hayo jana
alipokutana na wanachama wa umoja huo kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma
(UDOM), akidai kuwa amesikitishwa na kauli iliyotolewa hivi karibuni na
mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari, ya kulitaka jeshi la polisi
kuwakamata waliohusika na mauaji ya wanachama wake, vinginevyo
wangelijitangazia uhuru wao.
Alidai kuwa kauli ya Nassari ni ya kibaguzi na yenye lengo la
kuchochea umwagaji damu, hivyo, lazima hatua zichukuliwe dhidi ya
viongozi wa aina hiyo.
Aliwaambia wanavyuo hao walioandamano kwa ajili ya kumpongeza Rais
Jakaya Kikwete kwa ajili ya mabadiliko ya baraza la mawaziri kuwa CCM
inalaani kauli hiyo kwani siyo kauli nzuri katika mwenendo wa kisiasa.
Hata hivyo, wakati Shigela akilalama, tayari viongozi wa ngazi ya juu
wa CHADEMA, wametoa maelezo kuwa huo sio msimamo wa chama chao, na
Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe, alisimama na kukemea kauli hiyo.
Kwa upande wake, Nasari amedai kuwa kauli yake haikuwa na lengo baya
na ililenga kuweka mabadiliko ya kihamasa katika mikoa hiyo ili wengine
waone wivu wa kimaendeleo kwa mikoa ya kaskazini ambayo inaonyesha
mabadiliko makubwa.
"Mimi ni mtu mdogo tu sina nguvu hata kidogo ya kutangaza uhuru huo wa sehemu yoyote ya nchi” alifafanua Nasari.